Psquare Ft. J.Martins- E No Easy

Friday, June 18, 2010

IS THIS WHERE THE VUVUZELAS CAME FROM????????



TANZANIA KUWA MWENYEJI WA RIADHA VIJANA KANDA YA TANO AFRIKA!!


Timu ya taifa ya riadha ya vijana chini ya umri wa miaka 20 yafanyiwa mchujo.
Mchujo wa kutafuta timu ya taifa ya riadha ya vijana chini ya umri wa miaka 20 watakaoshiriki mashindano ya riadha ya Afrika kanda ya tano yametimua vumbi leo hii kwenye uwanja wa taifa jijini DSM.

Akizungumuza wakati wa mchujo huo katibu mkuu wa chama cha riadha Tanzania (RT) SULEIMAN NYAMBUI amesema Tanzania watakuwa wenyeji wa mashindano hayo na wao watayatumia kwa ajili ya kuunda timu ya taifa ya vijana ambayo baadhi ya wachezaji wake watashiriki katika michezo ya Jumuiya ya Madola yatakayofanyika mjini NEW DELH nchini INDIA MWEZI OKTOBA mwaka huu.

Nao wanariadha waliobuka kidedea katika mbio za mita mia nne, mshindi wa kwanza MOHAM,ED CHARLES wa ARUSHA na mshindi wa pili JOSEPH MSILA wa DSM wamesema watafanya vyema katika mashindano hayo ya vijana ya Afrika kwani wamejiandaa vyema kuibuka na ushindi.

Mashindano ya riadha ya kanda ya tano kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 yampepangwa kufanyika kuanzia tarehe 22 hadi 25 kwenye uwanja wa Taifa na yatashirikisha wanariadha kutoka nchi za MISRI, ETHIOPIA, ERITREA, KENYA, UNGANDA,BURUNDI,RWANDA na wenyeji TANZANIA. Habari na picha kwa hisani ya www.janejohn.blogspot.com

FEDHA ZA SERIKALI ZITUMIKE KWA MALENGO!!


Wabunge wameishauri Serikali kutumia vizuri fedha za barabara ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa fedha zote zinazopelekwa Wilayani kwa ajili ya ujenzi wa barabara zinatumika kwa utaratibu uliopangwa.

Wakichangia hotuba ya Waziri Mkuu Wabunge hao pia wameiomba Serikali kutoa mafungu ya fedha mikoani kwa uwiano unaoweza kuwasaidia wananchi.

Akitoa mchango wake, Mbunge wa Lindi Viti Maalum, Mhe. Riziki Said Lulida amesema, Serikali haina budi kuwa macho na watu wanaoingia hapa nchini kwa kivuli cha wawekezaji kwani wengine huja nchini hata bila mtaji wa kutosha badala yake waletwe wawekezaji wenye uwezo wa uwekezaji.

Mbunge wa Mafia, Mhe. Abdulkarim Shah ameitaka Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Uvuvi na Mifugo kuweka utaratibu wa kuwapatia wavuvi nyezo bora katika shguhuli ya uvuvi ili kuinua kiwango chao katika uvuvi.

Wabunge hao pia wameitaka Serikali kuendelea na utaratibu wake wa kutoa mbolea ya ruzuku kwa wakati kwa nchi nzima ili mkulima aweze kuongeza uzalishaji na tija

Wednesday, June 16, 2010

STEVEN KANUMBA AANZISHA MRADI WA KUNG'ARISHA VIATU ILALA!!


Muigizaji maarufu wa filamu nchini Steven Kanumba leo alifumwa na Camera ya FULLSHANGWE kiwa katika kaofisi kake kapya huko Ilala Boma akionekana yuko bize kwa kung'arisha viatu vya wateja wake, ambapo amekuwa akipata wateja wengi sana kiasi kwamba wapita njia hujaa na kuangalia ni kitu gani anafanya mwigizaji huyo.
Habari hii ilinifanya na mimi nivutiwe na kujua kile kilichomvutia mwigizaji huyo mpaka akaamua kwenda kuanzaisha kaofisi hako kapya ambako inaelekea kanamwingizia ngawila za kutosha kwa siku.
Hata hivyo Steven Kanumba alionekana kucheka wakati alipokuwa akinipa maelezo yake ambapo alisema hiyo ni moja ya Location ya filam u yake mpya inayokwenda kwa jina la
(More Than Pain) hebu tusubiri ili tuone itakuwaje wadau kaeni mkao wa kula.

MWAKALEBELA AELEZA MIKAKATI YAKE YA KIMAENDELEO IWAPO ATAMPOKEA MBEGA UBUNGE JIMBO LA IRINGA





KATIBU mkuu wa shirikisho la soka Tanzania Frederick Mwakalebela asema anagombea ubunge jimbo la Iringa mjini ili kumpokea mbunge wa sasa Monica Mbega(CCM) katika mchakato wa kufanikisha maendeleo ya jimbo hilo kama nilivyo fanya ndani ya TFF kwa kipindi kifupi cha uongozi wangu .

Mwakalebela aliyasema hayo leo nyumbani kwake Wilolesi mjini Iringa wakati akitangaza azma yake na sababu za yeye kugombea ubunge jimbo hilo mbele ya waandishi wa habari na wazee wa mji wa Iringa .

Alisema kuwa katika kampeni zake za kuwania nafasi hiyo kamwe hatajaribu kumsema vibaya mgombea mwenzake ndani ya CCM na nje ya CCM kwani amedai kuwa lengo la wagombea wote wa CCM na wale wa upinzani ni kujenga nyumba imara ndani ya jimbo hilo hivyo haoni sababu ya kugombea fito ama kuendesha kampeni chafu za kupakana matope.

Zaidi soma Tanzania Daima kesho ama tembelea http://www.matukiodaima.blogspot.com/ na http://www.mtotobaraka.blogspot.com/

HUJAFA HUJAUMBIKA BADO,HUYU NI MTOTO YATIMA ANATESEKA KWA KUKOSA MSAADA WA MATIBABU




Mtoto huyu ni mkazi wa Kijiji cha Mtitu wilaya ya Kilolo ambapo kwa sasa anasoma darasa la tano na hapa alipo anaishi na shangazi yake wazazi wake wote wawili walifariki dunia,kumbuka ikiwa leo ni siku ya mtoto duniani.

SAKATA LA OFISI KUCHOMWA MOTO MTANDAO HUU WABAINI SIRI NZITO,VIONGOZI WATATA WAKAMATWA



IMEBAINIKA kuwa ukimya wa tume iliyoundwa na mkuu wa wilaya ya Mufindi Evarita Kalalu kuchunguza tuhuma za viongozi wa serikali ya kijiji cha Igowole wilayani humo juu ya ufujaji wa mali za kijiji ndio uliopelekea hujuma kuchomwa moto kwa ofisi hiyo ya na nyaraka zote

Kuchomwa moto kwa ofisi hiyo ya serikali kunadaiwa ni kutokana na mkuu wa wilaya ya Mufindi Evarita Kalalu kuchewesha majibu ya tume aliyokuwa ameiunda kwa ajili ya kuchunguza ufisadi uliokuwa umefanyika katika kijiji hicho na viongozi wa serikali ya kijiji kwa kuuza miti ya kijiji kinyemela na fedha kuzitumia wao katika matumizi binafsi

Akizungumza namtandao huu juu ya tukio hilo mwenyekiti wa tume ya mkuu wa wilaya kijijini hapa Hosea Kyando alisema kuwa kabla ya watu hao wasiofahamika kuchoma moto ofisi ya kijiji juzi usiku mchana waliweka vipande vya sabuni katika mlango wa ofisi ya kaimu afisa mtendaji wa kijiji hicho ambaye ana wiki moja pekee toka aripoti kijijini hapo

Alisema kuwa kutokana na wananchi wa kijiji hicho kuukataa uongozi wa kijiji chini ya mwenyekiti wake Idphonce Kafuka ,mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mufindi alituma wakaguzi kwa ajili ya kukagua hesabu za kijiji hicho ambazo zilikuwa zikilalamikiwa na wananchi hao kiasi cha kufanya maandamano makubwa kuwataka viongozi wote wa kijiji kujiuzulu.

Hata hivyo viongozi hao hawakuweza kujiuzulu zaidi ya mkuu wa wilaya hiyo kuingilia kati suala hilo kwa kuunda tume ya kuchunguza malalamiko ya wananchi tume ambayo iliwasilisha ripoti yake ndani ya muda uliopangwa japo hadi sasa ni siku 14 zimepita bila mkuu wa wilaya kufika na kutoa ripoti ya uchunguzi wa tume hiyo kama alivyoahidi.
Hivyo alisema kuchelewa kutolewa kwa majibu ya tume hiyo ndiko kulikowakwaza zaidi wananchi hao ambao walilazimika kufunga safari hadi kwa mkuu wa mkoa wa Iringa Mohamed Abdulaziz kufikisha malalamiko yao na kuomba tume ya mkuu wa wilaya kutoa majibu yake.

"Hapa kuna mawili yawezekana ni viongozi wanaotuhumiwa wameamua kufanya hujuma ya ofisi ili kupoteza ushahidi...ama yawezekana ni wananchi wameamua kuchoma moto ofisi baada ya kuchukizwa na ukimya wa mkuu wa wilaya dhidi ya tume yake"
Pia alisema wakati moto huo ukiteketeza ofisi juzi usiku kegere iligongwa na wananchi wote waliweza kufika kuzima moto huo ila viongozi hao wa serikali ya kijiji ambao wamekuwa wakipingwa na wananchi hawakuweza kufika hata mmoja .
Mwenyekiti huyo alisema kuwa hadi sasa tayari askari polisi wamefika katika kijiji hicho kwa ajili ya kuchunguza tukio hilo japo na viongozi watatu akiwemo mwenyekiti na afisa mtendaji wamekamatwa na polisi kuhusiana na tukio hilo.
Mkuu wa wilaya ya Mufindi Bibi Kalalu alipoulizwa na mwandishi wa habari hii juu ya tume hiyo kuundwa na kushindwa kutolewa majibu kwa wakati alisema kuwa kwa sasa yupo jijini Dar es Salaam kwa matibabu na hawezi kulizungumzia zaidi suala hilo kutokana na matatizo ya kifanya yanayomsumbua huku mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo ya Mufindi Limbaksye Shimwela hakuweza kupatikana kuzungumzia tukio hilo.

MBAGALA HATA KAMA GARI TUPU LAZIMA ABIRIA WAKE WAINGILIE MADIRISHANI


Abiria wa Mbagala jijini Dar es Salaam wakigombea kuingia katika daladala eneo la Kariakoo leo jioni ,daladala ambayo hata hivyo haikuwa imejaza abiria , abiria hawa na Mbagala wamezoea kusukumana na kuingilia madirishani katika daladala hata kama daladala husika haijajaza abiria kwani ukiwa mkazi wa Mbagala lazima uwe na mbio za kufukuza daladala na uwe shapu wa kutumia nguvu kuingia mlangoni mwa daladala

Monday, June 14, 2010

Ujerumani yaanza vyema kwa kuibamiza Australia 4-0!!





Wafukua kaburi na kuiba viungo vya albino!


Watu wasiojulikana wamefukua kaburi alimozikwa mlemavu wa ngozi (albino) usiku wa manane wilayani Biharamulo na kuondoka na mkono na mguu wake huku masalia mengine yakiachwa ndani ya jeneza juu ya kaburi lake.

Habari kutoka eneo la tukio mkoani Kagera, zinaeleza kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa kuamukia Juni 10, mwaka huu katika Kijiji cha Nyakashenye wilayani Biharamulo.


Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi mkoani Kagera,kaburi lililofukuliwa ni la Lightness Laurian (29) alifariki dunia Januari mwaka huu.

Alisema watu hao walifukua kaburi na kutoa jeneza lake kisha wakalifungua na kuchukua viungo walivyovihitaji na kuondoka navyo.

Jeshi la polisi mkoani humo linaendesha msako mkali kuwasaka watu waliohusika na hadi sasa hakuna mtu anayeshikiliwa kuhusika katika tukio hilo.

Sijadiss wabongo- Dknob


Inocent Sahani a.k.a D Knob ameibuka na kukanusha habari zilizoandikwa na gazeti moja litokalo kila wiki mara mbili kuhusu shutuma za kuwa wabongo wamem-diss.

Kwa njia ya ujumbe mfupi wa maandishi wa simu D Knob alisema hata siku moja hawezi kuwa - diss wabongo kwani bila wao yeye asingekuwepo alipo leo hii na kwa mantiki hiyo hizo habari hazina ukweli wowote nakanusha kabisa.

Ujumbe wenyewe unasomeka kama ifuatavyo “Napenda kutangaza kuwa sijafanya interview na mwandishi wa habari yeyote hivi karibuni kwa hiyo nakanusha habari iliyoandikwa na gazeti la ijumaa la wiki mbili zilizopita kuwa wabongo wananidisi. Bila wabongo nisingekua hapa nilipo na wananisapoti na ndio maana Napata moyo wa kufanya vizuri” alisema D Knob

Huu ndio mwisho wa Kero za mikopo kwa wanafunzi- JK


FEDHA za kukopesha wanafunzi wa elimu ya juu kwa mwaka ujao wa fedha unaoanzia Julai mwaka huu, zitatengwa maalumu ili zipatikane wakati zinapohitajika na kukomesha uchelewaji wa fedha hizo.

Aidha, mwakani serikali inajipanga kuja na mkakati mwingine mahususi ambao wanafunzi wanaotaka kukopa, watakopeshwa na kujiwekea deni bila kujali uwezo wa wazazi wao.

Rais Jakaya Kikwete alisema hayo jana mjini hapa baada ya risala la wanafunzi wa elimu ya juu wa Mkoa wa Dodoma, kusisitiza matatizo wanayopata wanafunzi hao katika upatikanaji wa mikopo hiyo.

Katika risala hiyo, iliyosomwa na mmoja wa wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Egla Mamoto, wanafunzi hao pamoja na kumpongeza Kikwete kwa wazo lake la kujenga chuo hicho, lakini walisisitiza tatizo la kupata mikopo elimu ya juu.

“Tuko katika mtihani, lakini kwa kuzingatia kuwa wewe ndiyo chimbuko la elimu yetu, tumetenga muda kuja hapa,” alisema Mamoto na kushangiliwa.

“Maandamano haya ni kielelezo cha mapenzi yetu kwako na tunaunga mkono uwe mgombea pekee 2010 na tunazo sababu,” alisema.

Alitaja miongoni mwa sababu hizo kuwa ni utekelezaji makini wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2005 hasa katika elimu ambayo imewagusa na kusimamia wazo lake la ujenzi wa UDOM.

“Ulitoa wazo, ukalisimamia, ukajenga chuo kikuu, kwa hili usiseme wacha sisi wenyewe tunaonufaika tukusemee. UDOM ina hadhi ya kimataifa, je kama si wazo lako, leo hii tungekuwa wapi?” Alihoji mwanafunzi huyo na kushangiliwa na wenzake.

Alisisitiza pamoja na mafanikio hayo wanafunzi wanapata matatizo ya kupata mikopo.

Akijibu hoja hiyo ya mikopo pamoja na nyingine zilizoainishwa katika risala hiyo, Rais Kikwete alisema nia ya kuanzisha Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) ilikuwa njema na wataiendeleza.

Alisema tatizo la kuchelewa kwa fedha za mikopo lilitokana na fedha hizo kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kabla ya kufika HESLB.

Kutokana na tatizo hilo, ambalo wakati mwingine wizara hiyo ilizitumia fedha hizo, sasa kutaundwa mfumo ambao fedha za mikopo hazitapitia wizarani, badala yake zitawekwa maalumu ziwe tayari kwa matumizi ya wanafunzi wakati wowote.

Mbali na mfumo huo, mwakani kutaundwa mkakati wa kukusanya zaidi ya Sh bilioni 700 kwa wadaiwa vyuo vikuu, ili wanafunzi wa elimu ya juu watakaohitaji mikopo, wapatiwe bila kujali uwezo wa wazazi.

Kuhusu ujenzi wa UDOM, Rais Kikwete alikiri kuwa ujenzi wa chuo hicho haukuwa katika Ilani ya CCM ya 2005, bali waliibadilisha ili kuanza ujenzi wa chuo hicho.

Alifafanua kuwa “katika Ilani imendikwa tutapanua elimu ya juu, lakini wao wakabadilisha kidogo na kuweka, tutajenga chuo kikuu.”

Kauli hiyo ya Rais, imekubaliana na hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, aliyoitoa wiki iliyopita kwamba UDOM haiko katika Ilani ya CCM.

Mlipuko waua watu watano Nairobi!!


Nchini Kenya, Watu 5 wamethibitishwa kufa na wengine zaidi ya 100 kujeruhiwa baada ya milipuko iliyotokea jana katika mkutano wa kupinga katiba mpya inayopendekezwa.

Mkutano huo ulikuwa umepangwa na viongozi wa kidini Mjini Nairobi na ulihudhuriwa na maelfu ya watu wakiwemo wanasiasa. Polisi wanasema uchunguzi unaendelea na bado hawajui kilichosababisha milipuko hiyo japo huenda ikawa bomu ya kujitengenezea nyumbani.

Uchunguzi bado unaendelea kujua ni nani waliohusuka. Hata hivyo tayari makundi hasimu yameanza kuelekezeana lawama. Kundi la “NO” linalopinga katiba hiyo linadai kuwa huenda mlipuzi huyo alilenga kuhujumu mkutano wao na kulaumu polisi kwa kutotoa ulinzi wa kutosha kwao.

Waziri mkuu Raia Odinga hata hivyo amepuuza lawama hizo akisema kuwa kulikuwa na ulinzi wa kutosha. ” Tusihusishwe na milipuko hiyo kwani sisi kama serikali hatuwezi kuruhusu raia waangamizwe. Kwani sio sisi tuliotoa kibali cha kufanyika mkutano huo?” aliongeza Raila.

Wakati huo huo, polisi wamegundua maiti ya mtu mmoja ndani ya gari aina ya Prado, aliyepigwa risasi na kuuawa mahali pa milipuko hiyo. Haijulikani iwapo kisa hiki kina uhusinao wowote na milipuko ya awali na tayari uchunguzi umeanzishwa.

Sunday, June 13, 2010

Thabeet Online!


Hasheem Thabeet afungua website yake, kwa habari zaidi na mengineyo tembelea

www.hasheemonline.com

Namjua anayenichafulia jina ila sifwatilii mambo ya kiswazi- Aisha Madinda


Hatimaye Mnenguaji maarufu Aisha Madinda ameibuka na kuzoza na gazeti moja jijini Daresalaam akizikana picha zake za utupu zilizosambazwa mtandaoni na kwenye magazeti ya udaku a.k.a magazeti pendwa.

Akiongea na gazeti hilo alidai anamjua mtu anayemchafua hizo picha ametengeneza kwa sababu alimtolea nje

Ninamfahamu anayechapisha na kusambaza picha za ngono halafu anadai ni zangu, namuacha aendelee kwa sababu sipendi mambo ya kiswahili, mapenzi si lazima ni hiyari ya mtu kama umekataliwa tumia mbinu nyingine." mwisho wakunukuu.

Hivi karibuni kuna picha zilikuwa zimezagaa zikimuonesha mdada huyo akiwa mtupu huku kalewa zinazooneshwa alipokuwa nchini Afrika ya Kusini.

Watani wa Jadi kufinyana Agosti 14!



Agosti 14 ndani ya jiji la Lukuvu, ni siku ya ile mechi maalum ya kuwania ngao ya hisani kwa Watani wa jadi Simba na Yanga.

Naye Afisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage alisema kwamba timu hizo zitakutana baada ya Watoto wa Msimbazi 'Simba' kunyakua Ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita huku mahasibu wao wa jadi Yanga walimaliza wakiwa washindi wa pili wa ligi hiyo.

Alisema mbali na mechi hiyo, pia kutakuwa na mechi za kuwania ngao ya hisani katika mikoa yote nchini ambapo bingwa wa kila mkoa atacheza dhidi ya mshindi wa pili.

Kwani mwaka jana TFF iliwateua Mtibwa Sugar kutoka Morogoro kucheza dhidi ya mabingwa wa bara wa wakati huo, Yanga, baada ya Simba waliokamata nafasi ya pili huku Yanga kutoafiki kuvaana kwa madai kwamba hawakupewa taarifa mapema.

Mtibwa waliwachapa watoto wa jangwani 'Yanga' na kutwaa ngao hiyo ambayo huwaniwa wiki moja kabla ya kuanza kwa msimu wa ligi.

Na Agosti 21 mwaka huu ni kipindi cha kuanza kwa ile Ligi Kuu ya Tanzania Bara na itakuwa ni kipindi cha usajili wa wachezaji wapya

Mandela kamata jezi yako!!


Siku ya jana waliweza kumtembelea Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, na kuweza kumpa Jezi ya Ureno yenye jina la Mandela mgongoni.

Si wengine bali ni wale Winga wa Ureno Cristiano Ronaldo na Kocha Carlos Queiroz ndiyo walimtembelea Mandela nyumbani kwake na kwenda mpatia jezi hiyo.

Kwani Ronaldo na Queiroz walikuwa na nafasi ya kuzungumza na Rais huyo wa zamani wa Afrika Kusini, ni mara baada ya mwaliko binafsi kutoka kwa Rais huyo nyumbani kwake mjini Johannesburg.

Na walikuwa na furaha pia ya kumpatia fulana ya jezi ya Ureno, yenye jina la Mandela mgongoni na Na. 91, inayotaja umri wa mkongwe huyo.

Mandela anatimiza umri wa miaka 92 msimu ujao, na afya yake inazidi kudhoofika na anatokea mara chache hadharani.

Benki ya Dunia kuimwagia Bongo mkopo wa Mil. 914,200!


Kuanzia sasa itaanza kupokea Mkopo wa Sh. milioni 914,200 kutoka ndani ya Benki ya Dunia (WB), kwa madhumuni ya miradi mitano, mipya mitatu ikiwemo na mingine miwili.

Kwani utiaji saini wa mkopo huo ulifanywa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Ramadhani Khijjah na Mkurugenzi Mkazi anayewakilisha benki hiyo katika nchi za Tanzania, Uganda na Burundi, John Murray McIntire katika hafla iliyofanyika mjini hapa jana.

Na miradi mitatu mipya itakayogharimiwa na fedha hizo ni pamoja na Awamu ya Pili ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu, Mradi wa Kusaidia Sekta ya Usafirishaji na Mradi wa Kuboresha Miji.

Kwani miradi hiyo mitatu jumla imepewa takriban Sh. milioni 816,000.

Na Miradi inayoendelea iliyopata mkopo huo ni ule wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) na Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo (ASDP) ambayo kwa pamoja ilipata Sh. milioni 49,280.

Mbali na miradi hiyo..pia mradi wa Elimu ya Sekondari una lengo la kuboresha miundombinu ya shule, walimu na ufundishaji wa masomo ya Hesabu, Sayansi na Lugha pamoja na kuziongozea uwezo wa kifedha na utalaamu shule.

Kuhusu mkopo kwa ajili ya Mradi wa Usafirishaji, utasaidia kuboresha barabara kadhaa nchini vikiwemo na viwanja vya ndege.

Baadhi ya barabara ambazo alisema zitakarabatiwa kwa fedha hizo ni ile ya Korogwe- Same na ya Arusha hadi Minjingu.

Pia viwanja vya ndege vitakavyofaidika na pesa hizo ni vya Tabora, Kigoma na Bukoba.

Kuhusu mradi wa kuboresha miji, miji itakayofaidika na fedha hizo kuwa ni Mwanza, Arusha, Mbeya, Mtwara, Kigoma na Dodoma.

Na lengo kubwa la mradi huu ni kuboresha miji hii na hususan kuboresha huduma mbalimbali mijini, hususan upanuzi wa barabara.

Barabara zetu zimezidi uchakavu, walalama wanaTabata!!


Wakazi wa Tabata wameilalamikia Halmashauri ya Manispaa ya Ilala kufumbia macho suala la barabara chakavu zilizopo katika mitaa ya maeneo yao, kama ilivyo kwa barabara ndogo ya Savannah Relini yenye madimbwi makubwa ya maji, yanayoifanya isipitike.

Akielezea hali ya Barabara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Mazingira wa Kimanga Darajani Florence Mashaka, amesema madimbwi ya maji katika barabara hiyo ya Savannah Relini yamekuwa hapo kwa miaka 2 sasa, na pindi mvua zinaponyesha hali huwa mbaya sana.

Amesema Barabara hiyo husaidia kupitisha magari ya Vingunguti, Segerea, Ubungo, Kinyelezi na Buguruni nyakati za asubuhi na jioni, katika kipindi ambacho Barabara kuu ya Mandela inapokuwa imefurika magari.

Nao wajumbe wengine wa Kamti ya Mazingira sambamba na mkazi mmoja wa eneo hilo Paul Balua, wameitaka Manispaa kujitokeza mara moja kuokoa barabara hiyo, ili kuwezesha shughuli za watu kufanyika.

Tukabidhini washukiwa wetu- ICC


Mwendesha mashtaka mkuu wa Mahakama ya Kimataifa anaongeza juhudi kuhusu kesi dhidi ya raia wawili wa Sudan wanaotuhumiwa kwa uhalifu wa kivita.
Luis Moreno-Ocampo amelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuiamuru Khartoum kuwakabidhi wanaume hao kwa mahakama hiyo.

Raia hao wa Sudan walishtakiwa miaka mitatu iliyopita kwa uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu katika jimbo la Darfur, lakini baado wanaendelea kushikilia nafasi za juu serikalini.
Watuhumiwa walishtakiwa kwa mashambulizi katika vijiji kadhaa huko Darfur, ambayo yalisababisha mauaji ya watu wengi, ubakaji na watu kutoroka makaazi yao.

Bw Ali Kushayb ni kiongozi wa wanamgambo wanaolaumiwa kuhusika na uhalifu huo. Na Bw Ahmed Haroun, waziri wa zamani wa mambo ya ndani ambaye sasa ni mkuu wa mkoa, anashtumiwa kupanga mashambulizi hayo.

Mwezi uliopita majaji wa Mahakama ya ICC walitangaza kuwa serikali ya mjini Khartoum haiwajibiki ipasavyo kuwakabidhi watuhumiwa hao.

Sasa mwendesha mashtaka mkuu, Bw Ocampo alilihimiza Baraza la Usalama kushinikiza kwa nguvu ili kuhakikisha kukamatwa kwa watu hao.

Akijibu wito huo, Balozi wa Sudan katika Umoja wa Mataifa, Abdalmahmoud Abdalhaleem alimshtumu Bw Ocampo kwa kuwa na malengo yanayochochewa kisiasa, na kusema mpango huo unalenga kutatiza juhudi za amani katika jimbo la Darfur.
Bw Ocampo alisema mashambulizi dhidi ya raia yanaendelea kwa kiwango kikubwa Darfur, licha ya taarifa kusema kuwa hali imeimarika.

Obama na Cameron kujadili uvujaji wa mafuta!


Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron atajadili janga la kumwagika kwa mafuta katika Ghuba ya Mexico na Rais Barack Obama baadaye hii leo.
Bw Cameron amesema kuwa "ametatizwa na kuwa na wasiwasi mkubwa" kuhusu athari za kimazingira zilizosababishwa na kisima cha mafuta cha shirika la BP.
Lakini ofisi ya waziri mkuu ya Downing Street imesema mazungumzo ya simu na Rais Obama yatakuwa yenye manufaa.

Mhariri wa BBC wa masuala ya kibiashara Robert Peston alisema shirika la BP linaonekana kuitikia shinikizo za Marekanii na pia kusitisha malipo ya faida kwa wenye hisa wa shirika hilo.
Wakurugenzi wa shirika hilo watakutana siku ya Jumatatu kujadili uwezekano wa suala hilo.

Mwandishi wetu alisema " imechukua muda kwa bodi ya utawala wa BP kufikia uamuzi ikiwa Rais Obama anawataka kusitisha malipo kwa wenye hisa, na huenda hilo likawa jambo la busara ".

Shirika la BP litasitisha kutoa malipo hayo ya faida yenye thamani ya paundi 1.8bn, hadi hapo litaweza kujua ni kiasi gani cha fedha inatakiwa kulipa kutokana na janga hilo la kumwagika kwa mafuta na kuhakikisha kuwa inaweza kumudu gharama zote zinazohitajika.

Mwandishi wetu aliongeza kuwa hata kama gharama hizo zitapita paundi 20bn, wadadisi wanatarajia kuwa BP inahisi kuwa na rasilimali za kutosha kumudu gharama hizo.
Mafuta yamekuwa yakimwagika katika Ghuba ya Mexico tangu mtambo wa kuchimba mafuta chini ya bahari kulipuka tarehe 20 mwezi April katika jimbo la Louisiana, na kuuwa wafanyakazi 11.

Kiasi cha mapipa 40,000 ya mafuta yamekuwa yakimwagila kila siku hadi tundu lililokuwa linavuja kuzibwa tarehe 3 mwezi June.
Bw Cameron na Chancellor George Osborne wamekiwshazungumza na Mkuu wa shirika la BP, Carl-Henric Svanberg, kuhusu janga hilo.

England yabanwa na watoto wa Obama!!



Mechi kati ya ENGLAND na USA iliyofanyika katika kiwanja cha Rustenburg - Royal Bafokeng Stadium.

Haikuweza kuzaa matunda kwa Waingereza ambao toka awali walionekana wamepania sana na kujiandaa vyema katika mechi hiyo na huku asilimia kubwa ya mashabiki na wapenzi wa soka wa timu hiyo walikuwa na mategemeo makubwa na timu hiyo,baada ya kushindwa kuzitumia nafasi vyema ambazo zingeweza kuzaa matunda na kujikuta wakipoteza nafasi hizo.

Na hatimaye ENGLAND wakijikuta wakitoka sare ya goli 1-1 na USA, Goli hilo kwa upande wa ENGLAND lilifungwa na mchezaji STEVEN GERRARD mnamo dakika ya 4 na kwa upande wa USA waliweza kurudisha bao hilo lililofungwa na mchezaji CLINT DEMPSEY mnamo dakika ya 40.

Na katika mechi hiyo mchezaji TIM HOWARD alichaguliwa kuwa MAN OF THE MATCH.

Saturday, June 12, 2010

Enhe elezea kwanini ulivamia uwanja wa Taifa na kumpa Kaka mahug ya kutosha!


Siku chache baada ya Shabiki wa soka Nagari Kombo (21) kuvamia katikati ya wanja la Taifa, jijini Dar es Salaam wakati mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, na Brazil ikiendelea, ameanika sababu za kufanya hivyo.

Alichofanya kijana huyo akiwa peku huku akionekana kama mtu aliyepagawa, alichomoka kutoka upande wa mashariki mwa uwanja na kumfuata Kaka kisha kumkumbatia huku Kaka naye akifanya hivyo na kumpigapiga mgongoni kuashiria kupokea salamu.

Huku umati uliofurika uwanjani ukipigwa butwaa usijue kulikoni, kijana yule akionekana hana madhara, aliendelea na safari yake huku akishangilia kufanikiwa lengo lake kabla ya kudakwa na askari polisi akiwa nje ya uwanja.

Licha ya kuwekwa chini ya ulinzi, kilichoonekana kwa Kombo, ni kufurahia kile alichokifanya cha kumfuata Kaka na kumkumbatia, ingawa sasa amejikuta akiangukia mikononi mwa Jeshi la Polisi.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Kanda Maalumu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Dar es Salaam, Naibu Kamishna (DCP), Suleiman Kova, kabla ya mechi hiyo, Kombo alijiwekea nadhiri kwamba Brazil watakapokuja nchini, atahakikisha anagusana na Kaka.

Kova alisema kwa mujibu wa kijana huyo, kwa vile alijua adha ambayo ingempata kwa kitendo kile, kabla hajaingia uwanjani, alisaula pochi, viatu na simu ya mkononi na kutekeleza azma yake.

Kijana huyo amewaeleza polisi kuwa hakuwa na nia mbaya zaidi ya kutimiza azma yake ili iwe kumbukumbu katika maisha yake.

“Amesema isingekuwa rahisi kwake (Kombo) kukubali Kaka ambaye amekuwa akimwona akicheza kupitia runinga aje katika ardhi ya Tanzania na kuondoka bila yeye kushikana naye,” alisema Kova.

Kijana huyo aliyetoa maelezo hayo katika Kituo cha Polisi cha Chang’ombe, hadi jana alikuwa anashikiliwa kwa kosa la jinai la kuingia sehemu isiyoruhusiwa (Trans-pass).

Kova alisema shabiki huyo alitumia mbinu ambayo askari asingeweza kugundua kwani wakati anashuka, alionekana kama anayekwenda kujisaidia, lakini ghafla aliruka uzio na kwenda uwanjani kutimiza lengo lake.

Hata hivyo, Kova alisema si tukio la ajabu kwani hutokea hata katika nchi nyingi licha ya ulinzi kutokana na wahusika kutumia mbinu kali katika kufanikisha malengo yao kama alivyofanya.

“Jamani ulinzi katika mechi hiyo uliimarishwa vizuri, kwa aina ya kosa la Kombo, lisingeweza kuzuilika kutokana na kutumia mbinu kali za kuhakikisha anamfikia Kaka,” alisema Kova.

Kova alitolea mfano wa tukio kama hilo katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kati ya Arsenal na Barcelona ambapo shabiki mmoja wa Arsenal alivamia uwanja na kwenda kumfunika Thiery Henry kwa bendera.

Akirejea katika tukio ya Kombo, alisema wakati askari wakiwa wanaagalia juu ya usalama wa jukwa la juu alianza kutoa viatu na pesa kwa kukabidhi marafiki wengine wakijua midadi ya soka imempanda na kumuacha na utaratibu wake.

Kova amesema ingawa ni tukio la kishabiki zaidi, lakini Jeshi la Polisi halina budi kufanya kazi yake kwa vile ni kosa ambalo pia liliwanyima haki wote waliokuwa wakimfuatilia Kaka uwanjani muda ule.

Brazil imerejea nchini Afrika Kusini tayari kwa kampeni ya kusaka ubingwa wa sita wa Kombe la Dunia ambapo ikiwa katika kundi G, itaanza kampeni Juni 15 kwa kukipiga na Korea Kaskazini.

Brazil iliyopangwa kundi hilo lenye pia timu za Ivory Coast na Ureno, mechi ya juzi dhidi ya Stars, ni ya sita kwake katika ardhi ya Afrika huku Zimbabwe iliyocheza nayo Juni 2, ikiwa ya tano.

Namba za ZNZ sasa Kimeo Bara!



Wale wenzetu na sie tuliojinunulia magari yetu ya bei chee Zenji (Zanzibar)..na kutanua kiulaini mjini na namba za huko za 'ZNZ' zilizokuwa zikitumika kitambo kidogo kabla hatujajiandaa kubadilisha namba hizo kwa kulipia kodi,tunaelezwa na TRA kuwa hatima yetu imefikia kikomo.

Mamlaka hiyo ya mapato (TRA) inadai kuwa imebaini kuwa kwa kutumia namba hizo zilizokuwa zikitumika na ndugu zetu wa kisiwani kitambo kilichopita...kabla hawajaingia kwenye mfumo wa namba kama za kwetu bara...tunakuwa tunakwepa kodi...na kutokana na hilo imetoa mwezi mmoja kwa wale wote wanaotumia namba hizo kuzisajili mara moja kabla bakora hazijaanza kutembea mitaani hahaha.

Ofisa Uhusiano Mkuu wa TRA, MacDonald Mwakasendile, alisema jana kuwa hatua hiyo inatokana na kuwapo mitaani kwa vyombo hivyo; magari, pikipiki na vingine ambavyo vina namba za usajili za ZNZ huku wamiliki wakijua kuwa wanakwepa kodi kwa kuwa hakuna wanakolipia maana namba hizo hazitumiki hata Zanzibar.

“Hatutaki kusumbuana na watu, tumewapa muda, maana mwingine anaweza kulalamika hakuwa anajua japo sheria inamtaka kufanya hivyo, mwezi mmoja unatosha na hatua nyingine zitachukuliwa maana mtu unaponunua gari au pikipiki, unapaswa ibadilishwe mara moja namba za usajili,” alisema.

Kwa mujibu wa tangazo la TRA lililotolewa na Idara ya Huduma na Elimu kwa Mlipakodi, kupitia vyombo vya habari jana, wahusika wanapaswa kuwa wameandikisha kwa mujibu wa Sheria ya Usalama Barabarani kifungu namba 30 cha mwaka 1973.

Waganga wa jadi wampigia magoti Pinda!


Chama cha Waganga wa Dawa Asilia Tanzania, kimempigia magoti bosi wa mawaziri , Mizengo P, kuwaonea huruma na kuwapa kibali ili waendelee kutoa huduma kwa wateja wao kama ilivyokuwa siku za nyuma.

Hayo yaliwekwa wazi na chairman wa waganga hao, Simba Simba,ambapo alisema hatua ya serikali kuwasimamisha kwa muda usiojulikana, imewaathiri zaidi kwa vile ndiyo sehemu yao ya kupata fedha za kuendesha maisha.

Kwa mujibu wa Simba,wananchi wengi wamekuwa wakipata taabu kupata huduma hiyo, hali ambayo imepelekea kuwepo kwa waganga wanaotoa huduma hiyo kwa siri katika maeneo mbalimbali.

Alisema, kuwepo na misingi au chombo cha kuwaunganisha waganga wote nchini kutasaidia kuwasiliana katika kufanya kazi zao na kuwabaini waganga wanaojihusisha na vitendo vya kuwaua watu wenye uelemavu wa ngozi (albino).

Alisema chama hicho kimeweka taratibu ambazo zitawapa miongozo ya kazi waganga wote watakaojiunga kwenye chama chao ili watambuliwe kuanzia ngazi ya kata, mtaa, kijiji, wilaya mpaka taifa.

Familia yaburuzana kwa sangoma!


Familia moja ya jijii imekumbwa na mgogoro mkubwa wa kutuhumiana hadi kufikishana kwa waganga wa kienyeji kupigiwa ramli baada ya mtoto wao kupotea katika mazingira ya kutatanisha.

Mtoto huyo, Deogratus Jumanne (6), mkazi wa Kiwalani, alipotea wiki mbili zilizopita baada ya kwenda kumsalimia bibi yake wa ukoo wa mbali, Binti Said, anayeishi Mbagala Kibonde Maji tangu Mei 20, mwaka huu, lakini ilipofika Mei 23, alitoweka nyumbani.

Wakati juhudi za kumtafuta mtoto huyo zikiendelea, familia hiyo iligawanyika makundi mawili ambapo mama mzazi wa mtoto, Nuru Seif, alikwenda kwa sangoma kushughulikia tatizo hilo lakini upande wa baba haukutaka kushiriki kwenda kwa sangoma.

Imedaiwa kuwa upande wa mama mtoto ulienda kwa waganga tofauti na kuambiwa kuwa mtoto huyo amechukuliwa na bibi yake mzaa baba anayejulikana kwa jina la Ester Nyagalu huku waganga wengine wakidai amechukuliwa na Binti Said wa Mbagala.

Kauli za waganga hao zilisababisha vurugu kubwa baada ya mama mzazi wa mtoto na ndugu zake, akiwamo kaka yake, Hashimu Seif, kumvamia bibi Nyagalu na kumtaka kuwapa mtoto ndani ya siku tatu.

Hata hivyo, siku tatu walizotoa ziliisha juzi huku bibi huyo akiwa kitandani akiumwa.

Kutokana na vurugu hizo, watoto wa bibi Nyagalu, ambao ni Job Nyagalu na Jumanne Loki, waliingilia kati kupinga kumhusisha mama yao mzazi na mambo ya kishirikina kuhusu upotevu wa mtoto wao huku wakidai kuwa aliyehusika ni bibi wa Mbagala, Binti Said.

Kwa mujibu wa baba mazazi wa mtoto huyo, Loki, alisema kwa mujibu wa maelezo ya binti Said alidai kuwa Mei 23, mwaka huu kulikuwa na sherehe jirani yake huko Mbagala ambapo ngoma za asili zilikuwa zikipigwa kuzunguka maeneo mbalimbali na inawezekana mtoto huyo alifuatana ngoma hizo na kushindwa kurudi kutokana na ugeni wa mazingira hayo.

Alisema kitendo cha mke wake kwenda kwa waganga kwa kushirikiana na ndugu zake huku wakimhusisha mama yake mzazi kilimkera sana ingawa awali aliamini kuwa huenda waganga wangebaini mtoto huyo alipo.

Wanawake wasomi CCM, Upinzani akuu!! Oyee!!


Wapinzani walalamikia wanawake wasomi kujiunga CCM.

Viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani wamelalamika kuwa wanawake wasomi hawataki kujiunga na vyama vyao badala yake wanakimbilia kujiunga kwenye Chama Cha Mapinduzi.

Hali hiyo inavifanya vyama hivyo kukosa wagombea makini na wasomi wa kuwasimamisha kugombea ubunge kwenye majimbo mbalimbali.

Wanasiasa hao wanalalamika kuwa wanawake wasomi wanaona ni kupoteza muda kufanya siasa katika vyama hivyo na kwamba ndio maana wanakimbilia CCM na wale ambao hawana mapenzi kwa chama hicho tawala wanaona njia pekee ni kujiunga kwenye asasi za kiraia.

Baadhi ya viongozi wa vyama hivyo waliohudhuria warsha ya kuhamasisha viongozi wa vyama vya siasa kuhusu mambo ya jinsia na uchaguzi, walisema wanawake wengi wasomi ambao wana mwelekeo wa kufanya siasa wanapenda kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Wanasiasa hao walisema wanawake wanapenda kujiunga kwenye chama hicho kwa vile wanaona huko hakuna kazi ngumu ya kufanya siasa kuliko ilivyo kwa vyama vichanga ambavyo bado vinafanya kazi ya kujiimarisha ili viweze kupata wafuasi wengi.

Warsha hiyo madhumuni yake yalikuwa ni kujadili namna vyama vya siasa vitakavyofungua milango kwa wanawake kujitokeza kugombea ili kutimiza lengo la kuhakikisha uwakilishi kwenye bunge unakuwa asilimia 50 kwa 50.

Mwenyekiti wa NLD Dk Emmanuel Makaidi alitoa mfano wa Anna Senkoro ambaye alijitokeza kugombea urais kwa tiketi ya PPT Maendeleo kuwa alilazimika kukihama chama hicho na kujiunga CCM baada ya kubaini kuwa kwenye vyama vya upinzani ni lazima atoe fedha yake kuendesha shughuli za chama.

“Huyu alilalamika kuwa wakati anaumwa hakupata msaada kutoka kwa chama chake, ila kwa vile Rais Jakaya Kikwete alimsaidia wakati anaumwa akaona ni bora amfuate huko…zile shida za kukosa usingizi kufikiria utapata wapi fedha wanawake hawataki hayo,” alisema Dk. Makaidi.

Watoto wa Madiba wawabania wamexico!!



Mechi ya ufunguzi leo kati ya SOUTH AFRIKA na MEXICO iliyofanyika katika kiwanja cha Soccer City Stadium Johannesburg.

Haikuweza kuzaa matunda kwa wenyeji baada ya kushindwa kuzitumia nafasi vyema ambazo zingeweza kuzaa matunda na kujikuta wakipoteza nafasi hizo na kukosa magoli mengi ya wazi.

Na hatimaye SOUTH AFRIKA wakijikuta wakitoka sare ya goli 1-1 na MEXICO, Goli hilo kwa upande wa wenyeji SAUZI lilifungwa na mchezaji SIPHIWE TSHABALALA mnamo dakika ya 55 na kwa upande wa mexico waliweza kurudisha bao hilo lililofungwa na mchezaji RAFAEL MARQUEZ mnamo dakika ya 79.

Na katika mechi hiyo mchezaji SIPHIWE TSHABALALA alichaguliwa kuwa MAN OF THE MATCH

Wachungaji, Sheikh Nusura wapeane mangumi!!


SAKATA la kuzika mwili wa mtoto wa Mchungaji wa Kanisa la FPCT, Maria Yona (19) aliyefariki baada ya kuchinjwa kama kuku na mama yake mdogo limeingia katika sura mpya baada ya wachungaji pamoja na Sherkh mmoja kutunishiana misuli.

Hatua hiyo imekuja siku moja kufuatia wananchi kugoma kuzika mwili wa mtoto huyo hadi pale uchunguzi wa siku tano kufanyika.

Mabishano baina ya wachungaji wa kanisa hilo na sherkh mmoja aliyejulikana kwa jina la Mti Mkali kufika nyumbani kwa baba yake mzazi ili kufanya miujiza.

“Mchungaji pamoja na familia yake walikubali kundi hilo kuingia ndani ili kuona mwili wa marehemu lakini kundi la wachungaji wa kanisa la FPCT waligoma kabisa watu hao wasiingie ndani ya nyumba ya hiyo.”

Mwenyekiti wa kijiji hicho Bw.Aron Joseph alisema mara baada ya kundi hilo kutaka kuingia ndani ili kuuona mwili wa marehemu ndipo wachungaji waligoma na kuwaamuru kundi hilo kuondoka katika eneo hilo .

Kundi hilo pamoja na wananchi zaidi ya 3,000 waliokuwepo nyumbani hapo ili kushuhudia miujiza hiyo walipigwa na butwaa baada ya kuona kuwa watu hao wamezuiwa na wachungaji kufanya kazi yao .

Alisema kundi la Mti Mkali waliamua kuondoka katika eneo hilo na kuacha wananchi wakiwa katika makundi makundi kila moja likitafakari nini cha kufanya.

Bw.Joseph alisema hatua ya kutokuzika mwili wa mtoto huyo ambaye alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika shule ya sekondari ya Makhojoa, awali ulileta kasheshe wengi wa wananchi wakitaka usizikwe mpaka uchunguzi ufanyike.

Alisema ndipo wananchi walikusanyika katika makundi matatu kundi la vijana, kinamama na wazee kila moja likipewa majukumu ya kutafakari nini kifanyike.

Mara baada ya makundi hayo kukaa pamoja na kuleta mrejesho wa makubaliano ilionekana kila kundi lilitaka uchunguzi wa kina ufanyike kwani mazingira ya kifo cha mtoto huyo ni ya utata.

Hata hivyo ndipo ulizuka mjadala kijijini hapo ambapo wachungaji wa kanisa la FPCT, waislamu pamoja wa wazee waliingia katika maombi maalum ili kubaini chanzo cha kifo hicho.

Bw.Joseph alisema katika maombi hayo ndipo muumini wa kanisa la FPCT mwanamke mmoja alisema ameona maono kuwa Maria hajafa bali amefichwa sehemu na kwamba kilichopo ndani sio maiti bali ni gogo.

Alisema mwanamke huyo ambaye hata hivyo hakuweza kumtaja jina, juzi katika mkutano baina ya mkuu wa Wilaya ya Singida Bw.Pascal Mabiti na OCD Bw.Ngunguru, alisema kuwa katika maombi yake, maono yake yanaonesha kuwa hakuna mtu aliyekufa katika nyumba ya mchungaji Yona Mbighii.

Hapo ndipo wananchi walimtaka kutoa ushuhuda wake kwenye mkutano huo kwamba amwemwona wapi Maria, ndipo viongozi wa dini pamoja na wazee walikubaliana kuwa amweleze DC maono yake hayo kwa siri.

“Hapo ndipo huyu mama alimnong’oneza DC juu ya maono yake na ndipo mkuu wa Wilaya pamoja na OCD walisema kuwa suala hilo watalishughulikia kisheria lakini marehemu azikwe.”Alisisitiza Mwenyekiti huyo wa kijiji.

“Lakini jambo la kushangaza ni kwamba jana asubuhi mwanamke huyo alitoweka hapa kijijini na hajulikani alipo na juhudi za kumtafuta bado zinaendelea ili aweze pia kuweka bayana maono yake hayo mbele ya wananchi wa kijiji hiki.”Alisistiza.

Baada ya mabishano ya siku nzima ndipo iliamuliwa kwamba mwili huo uzikwe, jambo ambalo wananchi walipinga na kuamua kumziria mchungaji Mbighii na kanisa lake marehemu ili waamue wenyewe kamawatazika au la lakini wananchi hawapo tayari kushiriki mazishi hayo.

Alisema baadae wachungaji pamoja na baadhi ya ndugu wa marehemu, waliuzika mwili wa mwanafunzi huyo jana majira ya saa 4:00 asubuhi maziko ambayo yalihudhuriwa na watu takribani 30 tu.

Mwanafunzi huyo ambaye ni mtoto wa mchungaji wa Kanisa la FPCT lililopo katika kijiji cha Mipilo Tarafa ya IIongero, Halmashauri ya Wilaya ya Singida aliuawa kikatili juni saba mwaka huu na mama yake mdogo kwa kukatwa shingo kama kuku kutokana na imani za kishirikina

Mtoto wa Will Smith na Jackie Chan ndani ya bonge la movie!!







Usikose kuichek hii!! Dogo kafanya maajabu humo ndani, ama kweli mtoto wa nyoka ni nyoka..

Friday, June 11, 2010

Kombe la Dunia laanza Kwa Majonzi!!


Kitukuu wa Nelson Mandela Zenani Mandela amefariki dunia.

Afisi ya uhusiano mema katika wakfu wa Nelson Mandela imesema kuwa msichana huyo wa miaka 13 alifariki katika ajali ya barabarani iliyompata hapo jana akiwa njiani kutoka sherehe za mkesha wa kombe la dunia mjini Soweto.

Duru za polisi zimesema uwa dereva aliyesababisha ajali hiyo amekamatwa.

Huku hayo yakiarifiwa, mechi ya kwanza kabisa ya kombe la dunia kuwahi kufanyika barani Afrika inatazamiwa kuanza wakati wowote kati ya wenyeji Afrika Kusini na Mexico.

Timu 32 zinachuana kuwania kombe hilo baada ya mwezi mmoja na aliyekuwa rais wa Afrika Kusini Nelson Mandela anatarajiwa kuhudhuria sherehe ya ufunguzi leo jioni.

Sawa Mheshimiwa yuko salama ila magari yanahitaji kazi ya ziada!


IKULU imewatoa wasiwasi wananchi kuhusu usalama wa Rais Jakaya Kikwete na kuwahakikishia kuwa mkuu wa nchi yuko katika mikono ya watu makini, salama na wazalendo wanaoifahamu kazi yao.


Hayo yalisemwa Dar es Salaam jana na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Salvatory Rweyemamu, wakati akifafanua kuhusu tukio la magari matano yaliyokuwapo kwenye msafara wa Rais mkoani Kilimanjaro kupatwa na hitilafu na kushindwa kuwaka wakati wa ziara yake wiki hii.

Akifafanua kuhusu tukio hilo lililotokea Juni 8, mwaka huu, alisema sehemu ya magari ambayo ilikuwa yatumike kwenye msafara huo, yakiwa katika utaratibu wa maandalizi ya kumpokea Rais Kikwete katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), yalipelekwa katika kituo cha mafuta cha Rafiki.

“Baada ya kujazwa mafuta magari matatu kati ya hayo matano, yalikataa kuwaka, baada ya kuona hivyo, uamuzi ulichukuliwa wa kutoyawasha kabisa yale magari mengine mawili,” alisema Rweyemamu.

Hata hivyo, alisema kituo kilichotumika ni moja ya vituo ambavyo vimekuwa vinatumiwa kujaza mafuta ya magari ya Rais siku nyingi na kwamba uamuzi wa kuyajazia mafuta magari hayo katika kituo hicho haukuwa wa kushtukiza ama kubahatisha.

“Ukweli ni kwamba uamuzi wa wapi pa kujaza mafuta magari ya Rais, si wa madereva, bali huanzia ngazi za juu,” alifafanua.

Alisema kinachofahamika ni kwamba wakati magari hayo yanaingia kujazwa mafuta kituoni hapo, yalikuwa mazima, imara na salama kwa ajili ya kumpokea Rais Kikwete aliyekuwa anatokea Dar es Salaam na kwamba tatizo lilianza baada ya kujazwa mafuta hayo.

Hata hivyo, Rweyemamu alisema pamoja na hitilafu hiyo, msafara wa Rais ulipokelewa kama ilivyopangwa bila tatizo lolote kutokana na misafara ya aina hiyo mara zote huwa na mipango mbadala ya usafiri yenye kiwango cha juu cha usalama.

Alisema magari yaliyopata hitilafu hayakutumika kabisa katika msafara huo kwa kuwa yalikuwa yanasafishwa ambapo baada ya kusafishwa na kuwekewa mafuta mengine, yaliwashwa na kuwaka na yapo safarini kurejea Dar es Salaam.

“Uchunguzi wa tukio hili zima kwa sasa uko mikononi mwa vyombo vya usalama ikiwamo Polisi na Mamlaka ya Usimamizi wa Nishati na Maji (EWURA) na wakikamilisha uchunguzi wao, wananchi watajulishwa nini hasa kilitokea,” alisema.


Alisema tukio hilo haliathiri kitu chochote katika ziara hiyo na wala halikusababishwa na uzembe na kuhusu usalama wa Rais, hauna shaka yoyote na uko mikononi mwa watu wa kuaminika

Twanga kuazimisha Miaka Kumi!


Wazee wa Kisigino Twanga Pepeta bendi maarufu sana na ya muda mrefu inatarajia kutimiza miaka 10 toka kuanzishwa kwake kwa style ya kipekee ndani ya uwanja wao wa nyumbani pale Leaders Club.

Mkurugenzi wa ASET, Asha Baraka “Jiwe” alisema kuwa pamoja na kusheherekea miaka hiyo Kumi lakini pia kutakuwa na uzinduzi wa album yao mpya na ya Kumi pia inayojulikana kama “Mwana Dar es Salaam”

“Kutakuwa na maandamano ambayo yataanzia ofisi zetu zilizopo Kinondoni mpaka viwanja vya Leaders ambako kutakuwa na bonanza ambalo litakuwa na michezo mbalimbali kuanzia kuvuta kamba, mbio za kuku, mpira wa wavu kwa wanawake, mpira wa miguu na zaidi ya hilo kutakuwa na burudani mbalimbali za wasanii wa kibongo na nje ya bongo ambao watasindikiza sherehe hizo” alisema Asha Baraka.

Soko la nyama nchini laelezwa kuimarika


Soko la nyama ya ngombe nchini limeelezwa kukua kwa kasi nzuri, kutokana na kuuza nje ya nchi kati ya tani 6 na 10, kiwango ambacho hakikuwahi kuuzwa katika kipindi cha nyuma.

Akielezea mafanikio hayo, Afisa mauzo wa Bodi ya nyama nchini Kaiza Kuwana amesema soko la ndani na nje ya nchi kwa sasa ni kubwa kwa bidhaa hiyo, na kwamba juhudi zinafanyika kuuza wanyama wetu katika nchi ya Kenya kwa njia sahihi zitakazoingiza fedha za kigeni kwa Taifa, tofauti na inavyofanyika kimagendo kwa sasa.

Amesema kilo moja ya nyama inauzwa hadi Dola 4.25 za Kimarekani, na kwamba iwapo uzalishaji utaendelea kuborewshwa, nchi itazidi kunufaika.

Ukarabati barabara za jiji wapamba moto



Zoezi la ukarabati wa maeneo yenye kasoro katika barabara za jiji la Dar es Salaam limeendelea kupamba moto katika Wilaya ya Kinondoni, ambapo leo shughuli za kuziba viraka chakavu vya lami katika barabara ya Sinza Makaburini ilifanyika.

Akielezea maendeleo ya zoezi hilo, msimamizi wa ujenzi huo Immam Mvungi amesema shughuli inayofanyika ni kuvunja sehemu zilizoharibika na kuweka vipande vipya, kupanua maeneo finyu ya barabara pamoja na kuzibua mifereji iliyoziba katika barabara hizo.

Aidha ameeleza kuwa lengo la hayo yote ni kuimarisha barabara hizo ili kuweza kuondoa msongamano wa magari, pale yanapolazimika kupunguza mwendo kutokana na mashimo pamoja na kupita upande mmoja wa barabara kutokana uchakavu wa upande wa pili.

JK awamwagia Twiga Stars Mamilioni!!




Rais Kikwete ametoa shilingi milioni 53 kwa ajili ya kambi ya ya timu ya Taifa ya wanawake TWIGA STARS kujiandaa na fainali za mataifa ya Afrika ya wanawake nchini AFRIKA KUSINI ameyasema hayo leo katika sherehe za kuwapongeza timu hiyo zilizofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.

Pichani ni Rais Jakaya Kikwete akiwa na wachezaji wa Timu ya Twiga Stars pamoja na viongozi wao.