Psquare Ft. J.Martins- E No Easy

Saturday, April 10, 2010

Mtoto Wa Malkia Wa Uholanzi Aahidi Kulisaidia Jeshi La Polisi



Na Mohammed Mhina na Athumani Mtasha, wa Jeshi la Polisi

Mtoto wa Malkia wa Uholanzi, Her Royal Highness Princess Maxima, amesema kuwa nchi yake itaendelea kutoa misaada ya kitabibu kwa Jeshi la Polisi nchini Tanzania na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.

Princess Maxima, alitoa ahadi hiyo jana jioni, wakati akizungumza kwenye mkutano wa Hadhara uliofanyika Makao Makuu ya Kikosi cha Afya cha Jeshi la Polisi Barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam.

Princess Maxima, ambaye pia ujenzi wa wodi ya watoto, maabara ya kisasa ya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali na kliniki ya ushauri nasaha kwa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi (CTC).

Amesema kuwa lengo la misaada hiyo ni kuleta matumaini zaidi kwa askari na watumishi wa vyombo vya ulinzi na usalama vya hapa nchini kwa kujali afya zao kwa kuboresha huduma za tiba kwa magonjwa ya Kifua Kikuu na Ukimwi.

Amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kusimamia kwa karibu shughuli za ujenzi na ukarabati wa majengo ya Hospitali hiyo Kuu ya Jeshi na nyingine zilizopo katika mikoa mbalimbali na vyuo vya Polisi hapa nchini.

Kabla ya mkutano wa hadhara Pricenss Maxima, alikutana na kufanya mazungumzo na kikundi cha kutoa huduma wagonjwa majumbani kwa watu walioathirika na ukimwi na kifua kikuu.

Awali Waziri wa Mambo ya Ndani Mh. Lawrence Masha amesema kuwa Serikali ya Uholanzi kupitia Shirika la Maendeleo linalohudumia miradi ya Afya kwa nchi za Afrika, Farm Access International (PAI) tayari imegharimia ukarabati wa Zahanati 26 zikiwemo 13 za Jeshi la Polisi na nyingine 13 za Magereza.

Amesema kuwa hadi kufikia mwaka 2011 kila mkoa utakuwa na na Hospitali moja kwa Jeshi la Polisi na nyingine kwa Jeshia la Magereza zenye viwango vya kisasa na huduma za magonjwa ya ukimwi na Kifua Kikuu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Inspekta Jenerali Saidi Mwema amesema kuwa mbali na ukarabati uliofanyika katika Hospitali Kuu ya Kikosi cha Afya Jijini Dar es Salaam pia umefanyika ukarabati wa zahanati za Polisi zilizopo katika mikoa ya Mwanza, Mbeya, CCP Mkoani Kilimanjaro, Arusha, Tabora, Dodoma na Zanzibar.

Princess Maxima ambaye amefuatana na ujumbe wa watu 30 kutoka idara na wizara mbalimbali za nchini Uholanzi wakiwemo waandishi wa Shirika la Habari la Uholanzi NOVA yupo hapa nchini kwa ziara ya kiserikali.

Naye Mkuu wa Kikosi cha Afya cha Jeshi la Polisi hapa nchini Naibu Kamishna (DCP) Neven Mashayo amesema kuwa zaidi ya ukarabati wa majengo, mpango huo pia unalenga katika kuinua na kujenga uwezo kwa watendaji wa afya katika Hospitali za jeshi la Polisi ili zitoe huduma bora kama inavyotarajiwa.

Amesema ukarabati huo umeshaghalimu zaidi ya shilingi milioni 700 na kwa sasa kitakacho fuata ni kuanzisha kitengo cha X-RAY na Kitengo cha huduma za tiba ya Ukimwi VCT na maabara ya kisasa ya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali yakiwemo ya Kifua Kikuu (TB).

Serikali ya Uhalanzi pia imefanya ukarabati katika Jengo la Kiliniki kwa akina mama walioathirika na virusi vya HIV pamoja na kujenga sehemu maalumu ya uteketezaji wa taka ngumu na laini zitokanazo na Hospitali hiyo.

No comments:

Post a Comment