Psquare Ft. J.Martins- E No Easy

Wednesday, March 24, 2010


IGP Said Mwema.

WAKATI habari za wizi wa kimafia wa Sh300 bilioni zikiwa zimeistua serikali, watu kumi wamekamatwa kwa tuhuma za wizi mwingine wa aina hiyo uliohusisha Sh360 milioni za benki moja nchini.

Kukamatwa kwa watu hao kumetokea siku moja baada ya gazeti la Mwananchi kuripoti wizi huo mkubwa unaotumia teknolojia ya mawasiliano ya kompyuta ambao ulifanyika kwenye benki nne kubwa nchini, taarifa iliyofanya Mamlaka ya Mapato (TRA) kuanza uchunguzi.

Mbali na taarifa za kukamatwa kwa watu hao, vyombo vya habari pia vimeripoti kukamatwa kwa mfanyabiashara mmoja aliyekuwa akifanya jaribio la kuiba kimafia Sh221 milioni kutoka benki ya NBC.

Taarifa kutoka vyanzo mbalimbali vya habari ambazo zilithibitishwa na msemaji wa Jeshi la Polisi, Kamishna Msaidizi Abdallah Msika zinasema watu hao walikamatwa kati ya Februari na Machi, katika msako wa jeshi hilo kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Shinyanga na Zanzibar.

Kukamatwa kwa watu hao kumetokea wakati benki zimekuwa zikihaha kubadili na kuboresha mifumo yake ya kuchukua na kutoa fedha kwa njia ya elektroniki kwa lengo la kukabiliana na uhalifu uliokithiri unaofanywa na watu walio ndani na nje ya nchi.

Akithibitisha kukamatwa kwa watu hao, Mssika alisema watano kati yao ni wafanyakazi wa benki hiyo (jina tunalo kwa sababu za kimaadili) na wengine ni kutoka nje ya benki hiyo na kuongeza: “Hadi sasa uchunguzi bado unaendelea.

“Wote wanatuhumiwa kwa wizi huohuo wa mtandao… baada ya kufanyika uchunguzi walibainika kuwa ni sehemu ya mtandao ambaon inatuhumiwa unahusika kwenye wizi huo.”

Kwa mujibu wa taarifa hizo zilizothibitishwa na Mssika, wizi huo ulifanyika katika kipindi cha kuanzia Januari lakini ulibainika kati ya Februari na ndipo uchunguzi ukaanza.

Msika alifafanua kuwa baada ya kufanyika uchunguzi ilibainika kiasi hicho cha fedha kilihamishwa kutoka tawi moja jijini Dar es Salaam na kupelekwa tawi jingine la mkoani Shinyanga.

Alisema baada ya kuhamishiwa tawi la Shinyanga, fedha hizo zilianza kuingizwa kwenye akaunti mbalimbali za wahusika ndipo baadhi yao waliponaswa.

“Fedha zilitoka tawi la Dar es Salaam na kupelekwa tawi la Shinyanga, baada ya kufika Shinyanga zilianza kuingizwa kwenye akaunti mbalimbali za watuhumiwa… tayari hao kumi wamekamatwa kuhusika na tukio hilo,” alifafanua msemaji huyo wa polisi.

Kuhusu kiasi cha fedha, alisema hadi sasa zimepatikana Sh319.5 milioni kati ya Sh360 milioni zilizoibwa na kwamba juhudi za kusaka nyingine na watuhumiwa zinaendelea.

Mssika aliongeza kwamba baada ya watuhumiwa wengine kukamatwa, watajumuishwa katika kesi inayowakabili watu hao kumi walio mikononi mwa polisi.

Katika hatua nyingine, Mssika alisema Jeshi la Polisi limetaka benki yoyote ambayo imekumbwa na tuhuma za wizi huo wa mtandao ziwasilishe taarifa zao polisi.

Mssika, ambaye alilirudia kauli ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Kamishna Robert Manumba kuhusu taarifa za wizi mkubwa katika mabenki matatu, alisema hadi sasa hawajapata taarifa hizo kuhusu kiwango kilichoibwa na benki husika.

Wizi wa mtandao umekuwa ukikua kwa kasi nchini kutokana na matukio yaliyozikumba benki na tayari kuna kesi mbalimbali zinazohusisha wafanyabiashara wa Morogoro, walioba zaidi ya Sh1 bilioni katika moja ya benki nchini.

Lakini vyombo vya usalama ikiwemo polisi na mamlaka za serikali zimekuwa zikijaribu kufunika uhalifu huo.

Juzi wataalamu wa kubaini uhalifu wa kughushi kutoka Afrika Kusini walikuwa jijini Dar es Salaam kuangalia wizi mkubwa katika moja ya benki kati ya tatu zilizokumbwa na wizi huo wa kimafia wa Sh300 bilioni.

Benki hiyo ambayo inatajwa kuwa iliibiwa kiasi hicho kikubwa cha fedha, kwa sasa imeanza kurekebisha mfumo wake wa usalama wa fedha, hali ambayo imekuwa ikisababisha usumbufu mkubwa kwa wateja wake kwa takriban wiki nne sasa.

Tayari maafisa wadogo wanne wa benki hiyo wameshaondolewa katika nafasi zao kwa ajili ya kupisha uchunguzi zaidi kubaini uhalifu huo na mtandao wake.

Uchunguzi wa wizi huo unahusisha pia maafisa waandamizi ambao wanatuhumiwa kuwa wanaweza kushirikiana na mtandao wa wahalifu wa kughushi kufanikisha wizi huo wa kimafia.

Mwaka 2005/2006 Benki Kuu (BoT) iliibiwa zaidi ya Sh133 bilioni katika akaunti moja ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) baada ya watu kughushi nyaraka zilizoonyesha kuwa walirithishwa madeni na makampuni ya nne na hivyo kujivunia mabilioni ya fedha.

Hadi sasa, wafanyabiashara kadhaa pamoja na wafanyakazi wa BoT wameshafikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya kula njama na kuiba fedha hizo,

Hata hivyo, baadhi ya walioiba hawakufikishwa mahakamani baada ya Rais Jakaya Kikwete kutoa msamaha kwa wale ambao wangezirudisha kabla ya Novemba mosi mwaka 2008.

Mbali na waliorejesha kiasi cha Sh70 bilioni, waliokwapua kiasi cha Sh40 bilioni pia hawajafikishwa mahakamani kutokana na wizi huo kuhusisha makampuni mengine yaliyo nje ya nchi na hivyo uchunguzi kuhitaji nguvu kubwa zaidi kuweza kuwabaini wahusika

No comments:

Post a Comment